MKUTANO MKUU WA 10 WA KAUKI

MKUTANO MKUU WA 10 WA KAUKI
Tangazo la Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI

KAUKI-Kidamali, Iringa

KAUKI-Kidamali, Iringa
Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI

Monday, December 8, 2014


HOTUBA YA UFUNGUZI WA MKUTANO MKUU WA 10 WA KAUKI, JUNI 28 – 29, 2014, KIDAMALI – IRINGA

 

Ndugu Mgeni Rasmi, Ndugu Wageni Waalikwa; Wanaukoo na Jamii yote inayounda KAUKI;

Ndugu Majirani, Marafiki na Jamii yote Iliyojumuika Nasi; Mabibi na Mabwana;

 

Kamwene…, Munogage…, Makasi…,

 

Awali ya yote, nimwombe Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, uzima na Baraka, awape nguvu, afya na amani, wote mliokusanyika katika Mkutano huu wa 10 wa KAUKI. Pili, nimwombe Mwenyezi Mungu, awaepushe na hatari, rapsah na ubaya wowote ulioelekezwa kwenu; awalinde kutoka saa hii ya ufunguzi wa Mkutano hadi kesho wakati wa kuhitimisha shughuli hii muhimu kwa mwaka huu 2014.

 

Tatu, nawaomba wote tusimame kwa dakika moja (1) kuwakumbuka ndugu zetu ambao wametangulia mbele ya haki kutoka mwaka jana hadi mwezi Juni mwaka 2014. Ndugu waliotangulia mbele za haki ni:

1.   Agnes Mapembe, Mtoto wa Marehemu Sandra Kivenule, Mjukuu wa Kavilimembe Tavimyenda Kivenule

 

Mwenyezi Mungu azilaze Roho ya Marehemu mahali pema peponi, Amina.

 

Baada ya utangulizi huo mfupi, ni furaha kubwa kujumuika na hadhara hii siku ya leo.  Ni matumaini yangu kuwa wote ni wazima wa afya na pia uwepo wenu unaonesha namna mnavyothamini shughuli hii muhimu itakayofanyika kwa muda wa siku mbili; yaani leo na kesho, hali kadhalika kuhakikisha kuwa Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI unafakiwa.   

 

Ni furaha iliyoje kuwa nanyi katika hadhara hii. Ni matumaini yangu kuwa, wote ni wazima wa afya na kuwepo kwenu pia kuonesha jinsi mnavyothamini shughuli ambayo tutaifanya kwa siku mbili, yaani leo na kesho katika kuhakikisha kuwa Mkutano Mkuu wa Kumi wa KAUKI unafanikiwa.

 

Ndugu Mgeni Rasmi;  nianze kutoa historia fupi ya umoja huu. KAUKI ni Umoja wa Ukoo wa Kivenule, ulioanzishwa rasmi mwaka 2005, kukabiliana na changamoto mbalimbali za maendeleo, zinazoikabili jamii inayounda umoja huu; hususani katika kujikwamua na ugumu wa maisha na pia kutumia fursa zinazopatikana ili kukabiliana na kuondokana na wimbi la umaskini, ujinga, maradhi na utegemezi. Umoja wa Ukoo wa Kivenule (KAUKI), ulianzishwa rasmi mnamo Desemba 17 - 18, 2005 Kijijini Kidamali. Harakati za kuanzishwa kwa KAUKI zilianza mwezi Februari 06, 2005 Jijini Dar es Salaam kwa kufanya mkutano wa kwanza wa mashauriano. Harakati nyingine na kuunda kamati za maandalizi zilielekezwa upande wa Kidamali, Ilole na Nduli. Kwa upande wa Kidamali, Mkutano wa kwanza wa maandalizi ya Mkutano Mkuu ulifanyika mwezi Mei ambapo wajumbe toka Dar es Salaam walishiriki katika majadiliano, kuchagua viongozi wa kuunda kamati ya maandalizi na kuhamasisha.

 

Ndugu Mgeni Rasmi; Umoja wa Ukoo wa Kivenule ulizinduliwa rasmi mwaka 2006, katika Mkutano Mkuu wa Pili wa Ukoo wa Kivenule uliofanyika tarehe 24 – 25 Juni 2006 katika Ukumbi wa Sanga Kijijini Kidamali, Iringa. Kuzinduliwa kwa Umoja wa Ukoo wa Kivenule, kulienda sambamba na uzinduzi wa Mfuko wa Ukoo pamoja na Kuipitisha Rasimu ya Katiba ya Umoja wa Ukoo wa Kivenule na kuwa Katiba Rasmi; hivyo kutoa fursa ya kuanza kwa utekelezaji wa shughuli na mipango mbalimbali ya maendeleo. Pia, pamoja na mambo mengine, katika Mkutano Mkuu wa Pili wa Ukoo, kulifanyika uchaguzi wa Viongozi wa Kanda, uchaguzi wa Walezi wa Ukoo na hivyo utendaji rasmi wa KAUKI kuruhusiwa kuanza.

 

Ndugu Mgeni Rasmi; Huu ni Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI; na tayari mikutano mingine Nane imekwisha fanyika, mitatu kijijini Kidamali na mkutano moja kijijini Irole, Nduli, Igowole-Mufindi na Jijini Dar es Salaam na Mikutano 2 Magubike,. Huu ni mzunguko mwingine tena baada ya kumaliza kanda zote. Pengine mkutano huu utashauri namna nyingine ya uendeshaji wa mikutano ya namna hii.

 

 

 

Malengo ya KAUKI

Ndugu Mgeni Rasmi; malengo makuu ya KAUKI ni kujaribu kwa kila hali kwa kutumia ujuzi na maarifa, kuinua uwezo wa kielimu, kiuchumi na kimaendeleo, kwa wanajamii wanaounda umoja huo, kwa kutumia rasilimali mbalimbali zinazopatika katika nchi ya Tanzania na hususani katika maeneo wanayoishi; ikiwa ni pamoja kuihamasisha jamii hii kufanya kazi kwa juhudi na maarifa ili kupunguza umaskini unaowakabili.

 

KAUKI imeanzishwa kukidhi shida na mahitaji ya jamii iliyounda umoja huu na hususani katika maeneo lengwa ya elimu, afya, uchumi na maendeleo, kwa kushirikisha mawazo, fikra, ujuzi na maarifa ya kila mwanaukoo, katika mikutano mikuu na mikutano midogo midogo, ambayo inaandaliwa na wanaukoo wenyewe. Kwa kukutana pamoja, fikra za kujenga, ujuzi, uzoefu, kujengewa uwezo na maarifa, huunganishwa pamoja na kisha kupanga mikakati mbadala ya kuweza kukabiliana na changamoto zinazojitokeza katika maisha.

 

Ndugu Mgeni Rasmi; malengo KAUKI ni mengi na baadhi yake ni:

·        kuwa na ofisi yake Kijijini Kidamali na pia sehemu nyingine za Kanda

·        Kuisajili KAUKI na kuwa na mfuko wa kusaidia ndugu katika elimu, afya na matatizo mengine. Tayari mfuko umeanzishwa na unaendelea kuchangiwa. 

·        kuwa na sanduku lake la posta, tovuti. Kwa sasa ina tovuti  inayopatika kupitia www.tagumwafoundation.wetpaint.com na inaboreshwa kupitia www.tagumtwa.blogoak.com  na www.kauki-kauki.blogspot.com   

·        Kuwa na Akaunti katika Benki – tayari imefungua katika Benki ya NMB, Iringa Mjini

·        kuwa na vitendea kazi mfano Kompyuta, Printa, Simu, Meza na Viti

·        kuanza kutoa elimu mbalimbali kwa wadau wake. Inatoa elimu katika mikutano yake

·        kubuni na kutekeleza miradi ambayo itawasadia wanajamii. Mpango wa Mradi wa Alizeti-Irole, ambao bado haujaanza kutekelezwa.

·        kuwa na kitengo cha Utaalam wa Kitaaluma na Kiujuzi ambacho kitafanya shughuli za kuiletea fedha KAUKI, pamoja na miradi mbalimbali. Ipo katika mchakato.

·        Kuchapisha kitabu toleo la kwanza cha Umoja wa Ukoo wa Kivenule kwa kipindi cha mwaka 2009-2013. Kazi inaendelea na taarifa mbalimbali zinaendelea kukusanywa.

 

Mafanikio

Ndugu Mgeni Rasmi; KAUKI imefanikiwa kufanya yafuatayo:

·        kuendelea kufanyika kwa mikutano mkuu. Mikutano Mikuu Tisa tayari imefanyika Kidamali mara tatu, Magubike mara tatu, Irole, Nduli, Igowole-Mufindi na mara moja moja.

·        kupanua wigo wa ushiriki kutoka Irole, Nduli, Itagutwa, Mgongo na Mufindi; Kilimanjaro, Dar es Salaam, Morogoro na maeneo mengine.

·        Kuongezeka kwa ufahamu na uelewa wa watu kuhusu KAUKI na mada zinazofundishwa

·        Kufahamiana baina ya wana-KAUKI kumeongezeka mara dufu

·        Kuanzishwa kwa Mfuko wa KAUKI

·        Imeanzisha blogs ambazo zinabeba taarifa mbalimbali za KAUKI na wana-KAUKI kwa ujumla.

 

Changamoto

Ndugu Mgeni Rasmi; Changamoto zinazoikabili KAUKI ni pamoja na

·        Ushiriki duni wa wanaukoo katika mikutano mikuu.

·        Kasi ndogo na moyo wa kuchangia mfuko wa kusaidia wanaukoo

·        Kutokidhi gharama za kuandaa mikutano hii kwa sababu michango inakuwa ni kidogo

·        Kutofikia malengo ya mipango tunayojiwekea

·        Ndugu wa mijini kuwa na mwamko mdogo wa kuunga mkono jitihada hizi

 

 

Matarajio katika Mkutano Mkuu wa 10 wa KAUKI

Ndugu Mgeni Rasmi; Kama Ratiba inavyoonesha, hayo ndiyo yatakayofanyika katika siku mbili za Mkutano Mkuu wa Kumi wa KAUKI. Lakini, tunategemea kuwa na Mada kadhaa ikiwemo ya Chimbuko Historia ya Ukoo ambapo tutaijadili kwa undani zaidi. Lakini pia, masuala mengine mfano elimu, maendeleo na ushirikiano wa dhati baina ya wanandugu yatapewa kipaumbele.

 

Utambulisho baina ya wanaukoo utafanyika kwa kina na kila ndugu/mwanaukoo atakuwa na kitambulisho ambacho atakivaa kifuani kwake. Kutakuwa na fursa mbalimbali kwa wanandugu kupeana uzoefu mbalimbali wa utafutaji wa maisha bora. Mbinu za kujiinua kimaisha zitafundishwa na wadau wenye uzoefu pamoja na aina mbalimbali za miradi ambayo ndugu wanaweza kufanya.

 

Tutakuwa na kipindi cha kupeana uzoefu wa shughuli mbalimbali za kiuchumi kutoka katika maeneo mbalimbali ambako ndugu wanaishi. Kama ilivyofanyika katika Mkutano Mkuu wa Tatu, Nne, Tano, Sita, Saba, Nane na Tisa wa KAUKI, maeneo yatakayotolewa uzoefu Kilimo, biashara na ajira kutoka katika maeneo mbalimbali. Kwa kupeana elimu ya ujasiliamali itasaidia kutufungua macho na hivyo kuongeza uwezo wa kufikiri na kwenda kutafuta maisha katika maeneo ambayo ni mbadala kwetu. Pia taarifa hizi zitawasaidia wanandugu toka maeneo mengine kupata mwanga wa shughuli mbadala zitakazosaidia kupata kipato na kuboresha maisha.

 

Matarajio ya Mbeleni

Ndugu Mgeni Rasmi; Mipango ya KAUKI kwa mwaka uliopita 2014 na 2015

·        Kuendeleza jitihada za kufungua ofisi Kidamali na kununua vifaa vya ndani ya ofisi kama vile kompyuta, printa na fenicha.

·        Kutafuta hati ya Kimila ya Eneo la Kihistoria la Mlafu

·        KAUKI kufuatilia kwa karibu suala la Elimu kwa Watoto katika Kanda

·        Kuchapisha kitabu cha historia ya wahehe ambapo ndani yake pia kutakuwa na taarifa za KAUKI.

·        Kuongeza wigo wa ushiriki katika mikutano; Kuhamasisha wana-KAUKI kuchangia mfuko

 

Hitimisho

Ndugu Mgeni Rasmi; KAUKI imeendelea kujikita katika kuongeza uangavu na weledi kwa wanaukoo kutokana na kutambua changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika dunia hii ya ushindani. Ugumu wa maisha, mfumuko wa bei, ukosefu wa ajira, na changamoto mbalimbali ambazo kila mwana-KAUKI anaiona, ameguswa nayo au kuathiriwa nayo. Tatizo la ufisadi wa raslimali za watanzania, rushwa katika huduma za jamii mfano kukosa dawa hospitalini, maji safi na salama, elimu duni na ukosefu wa ajira, vyote vinatuathiri sisi. KAUKI inaamini kuwa mwana-KAUKI mwenyewe ndiye mwenye uamuzi wa mwisho ya kuamua hatma na mustakabali wa maisha yake ya sasa na baadaye. KAUKI haitarajii maisha bora kwa kila mwana-KAUKI au mtanzania mwingine yataletwa na wanasiasa au watu baki waliopo nje ya nchi yetu. Jukumu la maendeleo ni letu sisi wenyewe. Ndio maana tunahimiza watu kujitoa kwa hali na mali kuuchangia mfuko wetu ili uweze kuisaidia jamii yetu katika nyanja zote za kiuchumi, elimu, afya na maendeleo.

 

Ndugu Mgeni Rasmi, baada ya kusema hayo machache, kwa niaba ya Kamati ya Maandalizi ya Mkutano Mkuu ya Kidamali, Iringa, inakuomba Ufungue Rasmi Mkutano Mkuu wa 10 wa Umoja wa Ukoo wa Kivenule (KAUKI).

 

Karibu Sana

 

Imetolewa na:

 

Ndugu Faustino Kivenule

Mwenyekiti wa KAUKI

Kwa Niaba ya Kamati ya Maandalizi ya Mkutano Mkuu  wa 10 wa KAUKI

Adam Kivenule, Katibu Mkuu - Umoja wa Ukoo wa Kivenule (KAUKI)
WAHEHE: Ungazija wa Wanyalukolo

KARIBU msomaji kwa mara nyingine tena katika safu yetu ya Ndivyo Ilivyo. Wiki iliyopita tuliitambua asili ya Wahehe wenye mchanganyiko wa Uhabeshi na niliwaahidi kumalizia simulizi zao kwa kuchunguza mchanganyiko wao na kizazi cha Kingazija.

 

Tukiendelea na baadhi ya makundi ya WanitoleWahabeshi’ ya Wahehe, ambayo sikuyataja wiki iliyopita, ni pamoja na Vahafiwa walioishi sehemu za Kalenga, Kipagala, Kihesa, Tambalangombe, Ibanangosi, Tipingi, Ikolofya, Nyambila, Kibebe, Welu na Isanzala. Mtawala wao alikuwa Mwalyelu aliyetawala Welu hadi Pawaga ‘Mavaga’ na Mwamwano Mwansige aliyetawala Wutinde.

 

Majina ya watu wa kundi hili yalitokana hasa na kufa kwao kwa wingi kwa njaa na maafa, hawa ni kina Mwamugovano, Mwamaliga, Mwamukemangwa na Mwamuhesa. Husalimiana ‘kamwene hafiwa’ au ‘kamwene muponela’ ila kina Mwachaula husalimiana ‘kamwene lugome’. Vanyatengeta ni kundi lililoshi maeneo ya Uzungwa, Kitelevasi na Lundamatwe.

 

Hawa walikuwa ni mafundi wa kufua chuma, walioishi kwenye milima yenye asili ya milipuko ili kutafuta mchanga wenye chuma, baadhi yao ni kina Mwachusi na Mwamuvange. Salamu yao ni ‘kamwene tegeta’ ila kina Kalinga husalimiana ‘kamwene higo’, wao hawali mbawala.

 

Vanyakilwa ni watu walitokea Kilwa na kuishi maeneo ya Mufindi, hawa ni kina Mwalwagi na Mwakihwele, salamu yao ni ‘kamwene kilwa’. Vasavila waliishi juu ya milima ya Welu sehemu za Makungu, Magubike na Matogalu, hawa ni kina Mwamfilinge na Mwakasike. Vadongwe ni kundi lililoishi pembezoni mwa vilima katika maeneo ya Uhambingeto, Ipogolo, Nyabula na Luhota.

 

Wao ni mchanganyiko wa Wanitole na Wasungwa na salamu yao ni ‘kamwene huvi’. Baadhi yao ni kina Mwamuyovela, Mwamaluvanga na Mwamukakilwa. Makundi haya ya Wahehe yanadhihirisha kuwa, wao ni mchanganyiko wa vizazi vya watu wa jamii tofauti tofauti. Hebu tuone mathalan, jinsi damu ya Kingazija ilivyoingia kwa Wahehe na kuleta utawala wa Muyinga, kizazi cha kina Mkwavinyika (Mkwawa).

Wenyeji wa asili wa Iringa kabla ya Mwamuyinga kuingia na kuanza kutawala, ni Wasungwa, ukiwaacha Wanitole kwa mujibu wa historia halisi iliyovurugwa na tawala za vikundi vya hao Wanitole.

 

Wasungwa huishi katika safu ya milima ya Usungwa iliyopo mashariki ya mji wa Iringa. Mwamuyinga ambaye pia ana majina ya Mbunsungulu, Mwakilyemikongi, Muhumba, Mdagaluhando na Lwimato, yaliyotokana na taabu alizozipata kutoka Ukaguru hadi Mahenge, lakini jina lake halisi ni Hasani Yusufu, mjukuu wa Hasani Hasani, mtu aliyetokea Ungazija kupitia Ushelisheli hadi pwani ya Afrika ya Mashariki, akitafuta vipusa, pembe za ndovu na kufanya biashara ya utumwa kama ilivyokuwa kawaida ya Waarabu wengi wakati huo.

 

Alifika Kilwa Kisiwani na kushinda vita alivyopigana na kulowea huko kwa kuoa mwanamke wa Kiafrika aliyemzalia mtoto aitwaye Yusufu Hasani, aliyerithi usultani wake hapo baadaye na kumuoa mwanamke wa Kiafrika pia aliyekuwa binti Mulimba na kuzaa nae watoto wawili wa kiume, Hasani au ‘Mbunsungulu’ na Ahmad.

 

Yusuf Hasani aliondolewa mamlakani na kuuawa na Wareno waliokuwa wanapiga vita utumwa. Hasani ‘Mbunsungulu’ na nduguye Ahmad walikimbilia Mafia walikopendwa sana na wenyeji wa huko na walianza kutawala huko, ambako Mbunsungulu alioa.

 

Wakati mkewe akisubiri kujifungua, taarifa za Wareno kutaka kuwafuata na kuwaangamiza baada ya kugundua kuwa wako huko, ziliwafikia kupitia kwa mjomba wao, Malik Sud, aliyenusurika kwenye mapambano Kilwa Kisiwani. Kwa hiyo, iliwalazimu Mbunsungulu, Ahmad na mjomba wao kukimbilia Ukaguru karibu na Kilosa.

Kabla ya kuondoka, Mbunsungulu alimuusia mkewe kuwa mtoto akizaliwa aitwe Wakinakuonewa. Mbunsungulu alioa tena huko alikokimbilia na mkewe alimzalia watoto watatu, Ngulusavangi, Mufwimi na Ngwila.

 

Mama huyo alihama na kukimbia na watoto wake kutoka Ukaguru kuelekea Upogoroni, maeneo ya Ulanga huko Mahenge, baada ya Mbunsungulu, Ahmad na mjomba wao, kuvamiwa na Waarabu na kuuawa.

Vijana hao watatu wakaondokea kuwa wawindaji hodari sana huko walikokimbilia na walikuwa hawanywi maji ya mito, kila jioni walichimba visima. Ugomvi uliowatenganisha ulitokana na jambo hilo pamoja na kitendo cha Ngwila kutangulia kuoa kabla ya kaka zake Ngulusavangi na Mufwimi bila ya idhini yao.

 

Kuna habari nyingi za vijana hawa wote watatu, lakini tutajihusisha zaidi na Mufwimi ambaye uzao wake ndio ulimleta Muyinga.

 

Mufwimi aliendelea na uwindaji akiwa na wafuasi wake Mwilapwa, Mafumiko na Mabiki pamoja na mbwa wawili; Ludoviko na Muhepapakwima.

 

Alisafiri hadi Dabaga katika maeneo ya Ng’uluhe akifikia kwanza Ikombagulu alikowaacha wafuasi wake kwa muda na kuendelea mbele kuwinda katika eneo lililotawaliwa na Mwamududa. Huyu bwana alikuwa na uwezo wa kuua nyati hata kumi kwa siku, aliichoma nyama porini na kuipaka chumvi na kumtumia mtawala Mwamududa na kwa kuwa watu wa huko hawakuwa wanaijua chumvi bado, Mwamududa alipoipata nyama hiyo iliyotiwa chumvi aliiona tamu sana.

 

Chumvi ilimfanya Mufwimi apendwe na kupewa ruhusa ya kuwinda atakavyo na alipokaribishwa, aliomba mahala pa kulala akapewa nafasi nyumbani kwa mtawala Mwamududa. Huko alianza kufanya mapenzi ya siri na binti wa Mwamududa aliyekataa kuolewa na wanaume wengi waliojitokeza kumposa, hatimaye alimpa mimba. Alipoambiwa juu ya mimba hiyo na yule binti, aliagiza mtoto akizaliwa salama akiwa wa kiume aitwe Mwamuyinga na akiwa wa kike aitwe Semuyinga.

Mwiko wake asile funo, mnyama mdogo wa porini jamii ya mbuzi na nyakihuko, mnyama afananaye na panya. Pia asiokote kuni za mti uitwao munyatomaa na kukokea moto. Mufwimi alitoroka usiku kwa kuogopa kuuawa na Mwamududa ambaye kumbe alipopata taarifa za ujauzito wa binti yake, alifurahi sana kwa kujua kuwa sasa angeolewa kirahisi. Mufwimi hakuwarudia tena wale wafuasi wake bali aliendelea kuwinda hadi huko Itamba, Usungwa alikouawa na nyati.

 

Wafuasi wake walipomtafuta, walipata taarifa za kuuawa kwake huko Itamba, lakini pia walipewa taarifa ambazo Mufwimi aliwasimulia wakazi wa huko juu ya binti wa Mwamududa aliyemwacha na ujauzito wake.

 

Waliamua kwenda huko kwa kujifichaficha, lakini walipodhihirika, walikaribishwa vizuri na kupewa makazi na mtawala Mwamududa aliyefurahi kupata mjukuu. Huyu Mwamuyinga mtoto wa Mufwimi, chotara wa Kimanga aliyekuwa jasiri tangu ujanani, alimrithi babu yake na kuanza kutawala sehemu hiyo ya Ng’uluhe akiwa ‘Mutwa’ wa kwanza wa kabila lililotoka nje ya Tanganyika.

 

Ni kutokea kwa huyu Muyinga wa kwanza ndipo ulifuatia mfululizo wa vizazi kupitia kwa watoto waliozaliwa, ambapo Maliga alimzaa Mudegela aliyemzaa Kilonge aliyemzaa Ngawona Lupembe aliyeuawa na mdogo wake Munyigumba, ambaye alianza kuitanua himaya ya Uhehe baada ya kushika utawala mnamo mwaka 1870.

Huyu aliwashinda kivita wababe wa Kinitole na kuyaunganisha makabila ya Iringa, watu waliokuja kuitwa Wahehe na wakoloni hapo baadaye kutokana na mlio wao wa kivita wanapotupa mikuki kwa kusema he he he! wakiashiria hatari.

Kutoka Mutwa huyu ndipo alifuatia kutawala Mukwavinyika, mtoto wa pili wa Munyigumba, ambaye jina lake mtawala huyu liliwashinda wakoloni kulitamka na hivyo kufupisha kwa kutamka Mkwawa.

 

Mkwavinyika alianza kutawala akiwa na miaka 19 na aliyapiga vita makabila yote yaliyozunguka himaya yake na kuwashinda watu kama kina Chabuluma, Mtwa wa Wangoni na Merere, shemeji wa Mtwa wa Wasangu. Mukwavinyika alipigana pia na wakoloni wa Kijerumani.

 

Msomaji, simulizi hizi za Wahehe ni ndefu sana na zenye mambo mengi mno, ikiwemo kujipa majina ya kujitapa kulikofanywa kwa idhini ya Mutwa baada ya kutenda matendo makuu, ushujaa wa kutupa mikuki, uwezo wa mbio za kufukuza maadui, dawa za ushindi wa vita nakadhalika. Kwa sasa hapa panatosha kumalizia simulizi hizi za Wahehe.